Saturday, May 30, 2009

Miaka 11 ya MV Bukoba, Watanzania Bado tunarudia Makosa!

Makala hii imeandikwa na Deus Bugaywa kuadhimisha miaka 20 ya Ajali ya MV Bukoba katika mtandao wa www.freemedia.co.tz. Nimeona ni muhimu kwani inatoa 'uamsho' na mbadiliko wa mtazamo jinsi tunavyoziangalia ajali kama nchi.Ni makala ndefu kidogo lakini yaliyomo ni ya muhimu sana. Tafadhali ifuatilie hapa chini:
LEO inatimia miaka kumi na moja tangu itokee ajali mbaya ya kuzama kwa meli ya mv Bukoba, iliyokuwa ikifanya safari zake kati ya Bandari ya Mwanza na Bukoba.
Kama zilivyo ajali nyingine nyingi kubwa, ajali ya kupinduka na hatimaye kuzama kwa meli ya mv Bukoba ilipoteza maisha ya mamia ya Watanzania na kuwasababishia hasara kubwa ya mali.
Umekuwa msemo wa kawaida sasa kuwa, kufanya kosa si kosa, bali kurudia kosa ndilo kosa. Kwamba mtu hujifunza kutokana na makosa.
Kwa kuzingatia msemo huu, Watanzania walitegemea kuwa baada ya kutokea kwa ajali hii mbaya katika Ziwa Victoria, ndio ungekuwa mwanzo wa kuchukua tahadhari ya juu kabisa kwa usalama wa vyombo vyetu majini.
Si tu ilitarajiwa hivyo lakini pia ahadi nzito nzito zilizotolewa wakati wa msiba huo wa kitaifa na Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, ambaye ndio tu kwanza serikali ilikuwa ikijiweka sawa madarakani, zilitoa faraja na matumaini kwamba ajali kama hii ingebaki kuwa simulizi katika historia ya Ziwa Victoria.
Umati uliojaa simanzi na majozi juu ya msiba uliosababishwa na ajali hiyo uliahidiwa na Mkapa kwamba, serikali itajizatiti kuchukua hatua za tahadhari za hali ya juu kuhakikisha usalama katika vyombo vyetu vya usafiri.
Kwamba serikali ingehakikisha usafiri wa majini na nchi kavu hauwi tena wa kubahatisha, na hatua madhubuti zitachukuliwa kuhakikisha ajali zinazozuilika haziwi tena chanzo cha mauti kwa wananchi wa nchi hii.
Sina hakika kama ahadi hizo za serikali zilikuwa za ‘kisanii’ kwa maana kwamba zilitolewa kwa kusoma ‘mood’ ya waombolezaji walikuwepo pale au zilikuwa za dhati kwa maana halisi ya neno ahadi.
Tena sina hakika vile vile kama zilitokana na kile kisemwacho wanasiasa mara nyingi ‘husema wasichokiimaanisha na humaanisha wasichokisema’.
Nilicho na uhakika nacho na ambacho ninakishuhudia kila uchao katika suala zima la usafiri wa majini na hasa ndani ya Ziwa Victoria ni kwamba safari za ziwani humo sasa si za uhakika kuliko ilivyokuwa miaka kumi iliyopita.
Kilichopo sasa ni kama serikali imekwenda likizo ya mbali na wala haina matarajio ya kurudi karibuni kuangalia mwenendo wa mambo ulivyo katika safari nyingi zinazohusisha vyombo vya usafiri ziwani humo.
Unaweza ukaonekana kituko kwa watu wenye akili timamu, ukisema kwamba pamoja na Ziwa Victoria kuwa moja ya rasilimali kubwa na msingi wa mhimili wa mapato kwa famili nyingi za wakazi wa Kanda ya Ziwa na hata kwa uchumi wa taifa, Ziwa Victoria sasa lina sifa moja kubwa ya kuwa kaburi la uhakika kwa wasafiri wanaolitumia.
Sababu ya kuwa na sifa hii ni moja ambayo mimi sipati kigugumizi kuiita uzembe wa vyombo vinavyohusika na udhibiti wa vyombo vya usafiri ziwani humo.
Imekuwa si habari ya kushangaza wala kusikitisha kwa wakazi wa eneo la Kanda ya Ziwa kila siku kusikia watu wanne au watatu wamekufa maji wakati mtumbwi wao ulipopigwa wimbi na kuzama na kusababisha mauti kwa watu hao.
Habari ya kushangaza ni iwapo zikitangazwa taarifa za kumalizika kwa wiki nzima bila watu kadhaa kufa katika Ziwa Victoria, chanzo kikiwa ubovu wa vyombo vya kusafiria.
Sina hakika hasa wajibu wa Sumatra na wakala wake katika kuhakikisha usalama wa wasafiri katika Ziwa Victoria ni kutoa makalipio na ‘kujitoa’ kuhusika, kila ajali inapotokea au ni kuhakikisha kuwa sheria na taratibu zinazotawala mienendo ya vyombo vya majini zinafuatwa ili kupunguza ajali na kuzuia kabisa zile zinazozuilika.
Itakumbukwa kuwa baada ya kupotea na baadaye kuzama kwa meli ya mv Nyamageni, baadaye ilidhihirika kuwa meli hiyo ambayo imetengenezwa maalumu kwa ajili ya kubeba mizigo, pia huwa inatumika kubeba abiria.
Zaidi iligundulika kuwa pamoja na kukiuka taratibu za usafirishaji kwa kubeba abiria badala ya mizigo, pia ilikuwa na matatizo mengi ya kiufundi, tukiacha yale ya kutokuwa na vifaa muhimu vya kujiokoa wakati wa hatari.
Lakini katika mshangao wa kila mtu utetezi wa SUMATRA ulikuwa, wa kulaumu wale walioiruhusu meli hiyo kuendelea na safari zake wakati ilishapigwa marufuku kusafiri majini muda mrefu.
Mambo yakaishia hapo, watu wakaandaa taarifa yao ya kujitetea, waliobahatika kuokota ndugu zao walioibuka majini baada ya kufa maji, wakaenda kuwazika na waliopata hasara wakajuta kuzaliwa, mambo yakaisha.
Hivi karibuni, taifa limenusurika kupata msiba mwingine mkubwa, Mungu ashukuriwe kwa kutuepusha na balaa hilo, baada ya boti ya mv Mlinzi kutoboka na kuzama wakati ikiwa imewabeba Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na viongozi wengine wa serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM) waliokuwa wakisafiri kwenda wilayani Ukerewe.
Kama kawaida yao Sumatra, hawakukawia kutoa taarifa kwa mfumo ule ule wa taarifa zao za kulaumu, kama ilivyokuwa taarifa yao baada ya kuzama kwa meli ya mv Nyamageni, taarifa yao ilieleza kuwa, boti hiyo mali ya Idara ya Maliasili mkoani hapa, ilipigwa marufuku kusafiri tangu mwaka 2005.
Mlolongo wa ajali hizi unaonyesha wazi kuwa wahusika waliokabidhiwa dhamana ya kuhahakisha hali ya usalama katika vyombo vya usafiri ziwani hapa, hawapo kazini, wako usingizini, huwa wanaibuka yanapotokea maafa, na kwa sababu usingizi unakuwa haujawaisha machoni, wanakurupuka na kusema lolote, na wanafanya hivyo kwa sababu wanajua hao wanaowatamkia kauli hiyo ni mbumbumbu.
Nimetafakari sana kabla ya fikra zangu kunielekeza huko, nimejiuliza bila kupata majibu kwamba hizi marufuku za Sumatra zina maana gani hasa?
Kwamba chombo kimezuiliwa kufanya safari kwa ajili ya usalama wa watu na mali zao, lakini kinaendelea na safari zake kama kawaida mpaka kinapata ajali, ndipo Sumatra wanaibuka tena na kukumbuka kuwa walikwishazuia chombo hicho kusafirisha abiria au mizigo.
Kauli kama hizi au kwa uhakika kama wanavyosema wao ‘ripoti’ zinawasaidia nini Watanzania na wale waliokaidi amri ya mamlaka hiyo halali iliyopo hapo ilipo kwa ajili ya kufanya kazi kwa niaba ya serikali?
Hivi inawezekanaje Sumatra walioaminiwa na serikali kuhahakisha usalama wa Watanzania na mali zao wanapokuwa wanasafiri katika Ziwa Victoria wanatoa maagizo muhimu sana kwa maisha ya Watanzania kisha hawafuatilii utekelezaji wake?
Jambo moja ni wazi kwamba hapa tatizo si wasafirishaji, bali ni Sumatra.
Ingawa sijui ni kwanini wenzetu wa Zanzibar waliwatimua jamaa hawa, wanaoitwa Sumatra wasifanye kazi huko kwao, lakini ninadhani sababu iliyowafanya wakafikia uamuzi huo ni kama hii ya kushindwa kutekeleza majukumu muhimu kabisa ya usalama wa Watanzania huku kikiwa ni chombo cha serikali ambacho ninaamini kina mamlaka yote ya kuhakikisha maagizo yake yanatekelezwa.
Mv Nyamageni na mv Mlinzi, ni ushahidi wa kutosha kabisa kuwa Sumatra wameshindwa kufanya kazi waliyopewa na serikali, meli hizi, ingawa zilizuiliwa na Sumatra kufanya safari zake, ziliendelea kufanya hivyo.
Na kama si kupata ajali, ina maana hadi hivi leo zingekuwa zinaendelea kufanya safari zake na kwamba Sumatra ambayo ilizipiga marufuku haipo.
Kwa ushahidi huo, Sumatra ni ya nini? Kuna faida gani kama si hasara ya kulipa watu mishahara ya bure? Na je, ni dhambi kwa Sumatra kufukuzwa kutoka eneo la Kanda ya Ziwa kama ilivyofukuzwa kutoka Zanzibar?
Pengine maneno haya yanaweza kutafsiliwa kuwa ni makali kutumiwa katika makala hii, lakini kwa watu makini, wenye kutafakari kwa sawasawa watakubaliana na mimi kuwa ukali wa maneno si mzito kama uhai wa Watanzania ninaoulilia.
Pamoja na kutokuwa katika kudhibiti vyombo vibovu visisafiri majini, Sumatra pia wameonyesha uzembe mkubwa katika kuhahakisha kuwa vyombo vya usafiri majini vinakuwa na vifaa vya kujiokoa.
Kwa kiasi kikubwa kunusurika kwa viongozi waliokuwa katika mv Mlinzi, kulitokana na wao kuwa wamevaa maboya, (life jackets) tangu mwanzo wa safari yao, vinginevyo haina shaka kwamba hivi sasa tungekuwa tunaongea habari nyingine.
mv Mlinzi inamilikiwa na Idara ya Maliasili hivyo kuwa na maboya ni jambo lilitorajiwa na wengi, lakini vyombo vingi binafsi vinavyofanya safari zake katika Ziwa Victoria havina kabisa maboya hayo na vile ambavyo vinayo hayatoshelezi abiria wanaosafiri na vyombo hivyo.
Na la kushangaza zaidi ni kwamba hata hayo maboya machache yaliyo katika baadhi ya vyombo hivi hayavaliwi na abiria.
Hili Sumatra inalijua, kwa sababu vyombo hivi vinatia nanga kila siku katika maeneo mbalimbali ya ufukweni mwa ziwa hili.
Inasikitisha kueleza ukweli kwamba idadi kubwa ya abiria ambao licha ya kutojua kutumia maboya hayo, lakini pia hawajui hata mahali yalipo ndani ya vyombo hivyo.
Ushahidi wa hili ni mmoja wa walionusurika katika ajali ya mv Mlinzi, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kagera, Pius Ngeze, aliyekaririwa akieleza kuwa licha ya kupewa maboya hayo kabla ya kuanza safari, hawakupewa maelekezo ya namna ya kuyatumia.
Ngeze anaeleza kuwa kutokana na kutojua kulitumia boya alilokuwa nalo, alijikuta likimfunika na laiti kama Anthony Diallo, Waziri wa Maendeleo ya Mifugo asingekuwa jasiri na kuthubutu kumvuta wakati boya hilo likimzamisha, sasa angekuwa marehemu.
Inasikitisha, jinsi Watanzania tunavyochezea maisha yetu, jinsi ambavyo tumeshindwa kujifunza kutokana na ajali ya mv Bukoba licha ya ahadi nyingi zilizotolewa wakati huo kuwa tahadhari kubwa itachukukiwa katika usafiri wa majini.
Kunusurika kwa viongozi wetu hawa kufa maji ndani ya ziwa lile lile lililozamisha ndugu zetu wengi na kuwazika humo, liwe fundisho kubwa, la pili, ni kuanza kuchukua tahadhari zote za kuhakikisha usalama wa usafiri katika maeneo mbalimbali ya maziwa na baharini.
Lakini pia tunapoadhimisha miaka 11 tangu maisha na mamia ya ndugu zetu yalipopotea ziwani, tukumbuke yale tuliyoahidi kufanya ili kuhakikisha tunaepuka uwezekano wa kutokea kwa ajali kama hiyo kwa mara nyingine.
Inawezekana tunakaribia kuchelewa lakini bado nafasi ya kujisahihisha tunayo, uwezo wa kurekebisha hali ya usafiri wetu pia tunao, na sababu za msingi kuchukua hatua za haraka kurekebisha hali ya sasa na kufanya safari zetu kuwa ni sehemu ya amani na si chanzo cha mauti tunazo.
Maadhimisho ya miaka 11 ya kumbukumbu ya ajali ya mv Bukoba, yazirejeshe nia zetu, katika dhamira ya dhati kuzuia ajali hizi ambazo kila siku zinaua Watanzania wenzetu.
Vinginevyo hatuwezi kukwepa kufananishwa na msemo wa sikio la kufa halisikii dawa.
Mungu awapumzishe pema peponi wale wote waliotutoka katika ajali ya mv Bukoba na awape faraja na matumaini wale wote walioondokewa na wapendwa wao katika ajali hiyo.
0754 449 421
drbugaywa@yahoo.com

No comments:

Post a Comment

blogarama - the blog directory
Directory of News Blogs
This blog gives information about accidents-vehicles,motorcycles,bycycles etc,also highlights the suffering of those involved in various accidents. It gives counselling to the accidents victims and information as to where they can get assistance be it legal or humanitarian.
Health blogs
eXTReMe Tracker